Awali ilijulikana kama “Elton Plateau" baada ya Mvumbuzi Fredrick Elton kupita eneo hili mnamo 1870. Mwaka 1960 Shirika la Chakula na Kilimo (FAO) lilichukua eneo hili kwa ajili ya ukulima wa ngano na ufugaji wa kondoo.
Kutokana na umuhimu wa eneo hili, wadau mbalimbali wa mazingira walipendekeza eneo hili litangazwe hifadhi ya Taifa ili kulinda umaridadi wa maua na mimea adimu ipatikanayo ndani ya eneo hili.
Mwaka 2005 Kitulo ilitangazwa rasmi kuwa hifadhi ya Taifa ikijumuisha sehemu ya eneo la shamba la mifugo; msitu wa Livingstone na bonde la Numbi kiasi cha kilomita za mraba 412.9 ndani ya mwinuko wa mita kati ya 2,100 na 3,000.
Hifadhi hii inasifika kwa kuwa na aina mbalimbali za maua zaidi ya aina 30 hupatikana Kitulo pekee na maeneo ya kusini mwa Tanzania.
Pia ndilo eneo pekee Tanzania ambapo ndege aim ya Tandawala machaka (Denhams Bustard) wana makazi. Wapo aina mbalimbali ya ndege kama vile Mpasua mbegu mweusi (Kipengere seed eater) na wengineo.
Jamii mpya ya nyani (Lophocebus Kipunji) waligunduliwa katika hifadhi ya Kitulo mwaka 2003.
Hifadhi hii ina uwanda wa tambarare, mabonde, vilima na maporomoko ya maji. Ndani ya msitu, kun miti aina ya “cidar” yenye urefu wa zaidi ya mita 50 na inakadiriwa kuwa mirefu kuliko yote duniani.
Kitulo inafikika kwa njia ya barabara. Vile vile Reli ya TAZARA hupita karibu na hifadhi ya Kitulo.
Kuna hoteli kadhaa mjini Mbeya na nyumba za kufik wageni katika kijiji cha Matamba.